BIBLIA INASEMAJE KUHUSU UCHEZAJI WA KAMARI?
Baadhi ya watu huona kwamba hakuna ubaya wowote 
kucheza kamari, lakini wengine huona kuwa zoea hatari.
Je, kuna ubaya wowote wa kucheza kamari?
WATU HUSEMA NINI?
Watu wengi huona kwamba kucheza kamari ni burudani isiyo na madhara 
ili mradi tu kufanya hivyo kunakubalika kisheria. Aina fulani ya michezo ya 
kamari inayokubaliwa kisheria kama vile michezo ya bahati nasibu inayofadhiliwa 
na serikali, imekuwa chanzo cha mapato kwa watu wengi.
BIBLIA INASEMA NINI?
Biblia haisemi moja kwa moja kuhusu kucheza kamari. Hata hivyo, 
inatoa kanuni mbalimbali zinazoweza kutusaidia kujua maoni ya Mungu kuhusu 
kucheza kamari.
Kucheza kamari kunahusisha kushinda pesa za watu 
wengine, jambo linalopingana na onyo la Biblia linalosema, “mjilinde na kila 
namna ya tamaa.” (Luka 12:15) Pupa huchochea watu kucheza 
kamari. Taasisi za michezo hutangaza kuhusu mashindano makubwa ya bahati nasibu 
ijapokuwa hawapendi watu wajishindie pesa hizo, lakini wanafanya hivyo wakijua 
kwamba watu huchochewa na ndoto za kuwa matajiri na hivyo kutoa pesa nyingi 
katika majumba ya kucheza kamari. Kamari huchochea watu kuwa na tamaa ya kutaka 
kupata pesa haraka badala ya kuwasaidia kujilinda na pupa.
Kucheza kamari kunahusisha roho hii ya asili ya 
ubinafsi: kushinda pesa walizopoteza wengine. Hata hivyo Biblia inatia moyo mtu 
“aendelee kutafuta, si faida yake mwenyewe, bali ile ya yule mtu mwingine.” (1 Wakorintho 10:24) Sheria moja kati ya 
zile Sheria Kumi inasema: “Usitamani . . . chochote cha mwenzako.” (Kutoka 20:17) Mcheza-kamari anapoazimia 
kushinda pesa, kihalisi anatumaini kwamba wengine watapoteza pesa zao ili yeye 
afaidike.
Biblia inatoa onyo kuhusu wale wanaotegemea 
bahati kama chanzo kikuu cha mafanikio. Katika Israeli la kale, kulikuwa na watu 
waliokosa imani kumuelekea Mungu na kuanza “kuandaa meza kwa ajili ya mungu wa 
Bahati Njema.” Je, ujitoaji wao kuelekea “mungu wa Bahati Njema” ulikubaliwa na 
Mungu? Hapana, kwa kuwa aliwaambia hivi: “Nanyi mliendelea kufanya yaliyokuwa 
mabaya machoni pangu, mlichagua jambo ambalo halikunipendeza.”—Isaya 65:11, 12.
Ni kweli kwamba katika nchi fulani, pesa 
zinapatikana katika michezo ya kamari iliyokubaliwa kisheria hutumika kulipia 
elimu, kuendeleza uchumi, na shughuli nyingine za kijamii. Lakini matumizi ya 
pesa hizo hayabadili njia ya upatikanaji wake, yaani, kupitia shughuli 
zinazochochea pupa na ubinafsi na zinazoendeleza wazo la kupata pesa kwa 
haraka.
“Usitamani . . . chochote cha mwenzako.”—Kutoka 20:17.
Mcheza-kamari anawezaje kuathiriwa kwa kucheza kamari?
BIBLIA INASEMA NINI?
Biblia inaonya kwamba “wale ambao wameazimia kuwa matajiri huanguka 
katika jaribu na mtego na tamaa nyingi za kijinga na zenye kudhuru, ambazo 
hutumbukiza watu katika maangamizi na uharibifu.” (1 Timotheo 6:9) Watu hucheza kamari kwa 
sababu ya pupa, na “pupa” ni mbaya sana hivi kwamba Biblia inaitaja kuwa 
miongoni mwa tabia tunazopaswa kuepuka kabisa.—Waefeso 5:3.
Kwa kuwa hukazia hasa kutajirika haraka, 
uchezaji-kamari humchochea mtu kupenda pesa jambo linalotajwa na Biblia 
kuwa “chanzo cha mambo mabaya ya namna zote.” Tamaa ya pesa inaweza kwa urahisi 
kuwa jambo muhimu zaidi maishani mwa mtu na kumfanya awe na mahangaiko mengi na 
kuharibu uhusiano wake na Mungu. Biblia inawataja kwa njia ya mfano wale 
walionaswa na upendo wa pesa kuwa “wamejichoma wenyewe kila mahali kwa maumivu 
mengi.”—1 Timotheo 6:10.
Pupa huwafanya watu wasiridhike na hali yao ya 
uchumi na hivyo kukosa furaha. “Anayependa fedha hatatosheka na fedha, wala 
anayependa mali hatatosheka na mapato.”—Mhubiri 5:10.
Mamilioni ya watu walioshawishika kucheza 
kamari wamekuwa waraibu wa mchezo huo. Makadirio yanaonyesha kwamba tatizo hilo 
limeenea sana, huku kukiwa na mamilioni ya waraibu wa mchezo huo nchini Marekani 
pekee.
Methali moja inasema hivi: “Urithi 
hupatikana kwa pupa mwanzoni, lakini wakati wake ujao hautabarikiwa.” (Methali 20:21) Kucheza kamari kumefanya 
waraibu wa mchezo huo kuingia katika madeni au kufilisika, kupoteza kazi, 
marafiki na kuharibu ndoa. Kutumia kanuni za Biblia kunaweza kumsaidia mtu 
kuepuka madhara ya kucheza kamari na kumfanya awe na furaha maishani.
“Wale ambao wameazimia kuwa matajiri huanguka katika jaribu na mtego na tamaa nyingi za kijinga na zenye kudhuru, ambazo hutumbukiza watu katika maangamizi na uharibifu.”—1 Timotheo 6:9.

Comments
Post a Comment