Kushindana na Shetani
Maana ya jina Shetani ni
 adui, au mpinzani.  Baalam alipopingwa na malaika (Hesabu 22:22), 
malaika yule alifanya kazi kama Shetani (ingawa hakuwa Shetani, ila 
kupinga huku ni kama afanyavyo Shetani).  Shetani ni adui 
anayepinga.  Anapinga Uungu usionekane.  Maahali popote palipo pema 
atapapinga na kuleta ubaya. Palipo na nuru atapinga na kuleta giza. 
Palipo na kweli atapinga nakuleta uongo, palipo na uzima atapinga na 
kuleta mauti.  Maandiko yanasema Mungu alimwondokeshea Sulemani adui 
mwingine aitwaye Rezoni (1 Wafalme 11:23).  Adui huyu alimpinga 
Sulemani, kama Shetani afanyavyo.  Roho ya mpinga Kristo (1Yohana 4:3), 
ni roho ya Shetani, inapingana na Mungu na uungu duniani (2 
Wathesalonike 2:3-4).
Yesu  alishamshinda
 Shetani kwaajili yetu (1Wakorintho 15:57). Amemshinda na ametupa 
kushinda kwake. Kumshinda Shetani huku ni kushinda ushetani, yaani 
upingamizi wake. Hata hivyo Adui amebaki na kitu kimoja kinaitwa HILA. 
Kwa Kiyunani hila ni methodaeias, tafsiri yake ni mbinu za kulaghai na kutega mitego.  Silaha tunazivaa ili kupinga hila na sio nguvu za Shetani,
 Shetani nguvu hana kwa njia ya Yesu. Yesu alimharibu kabisa msalabani! 
Hatupigani naye, Yesu alishapigana naye akamshinda.  Sasa tunashindania 
ushindi wake, tunahakikisha unasimama wakati wote, hatuutafuti tunao, 
tunashindana usimame wakati wote.
YESU AMESHASHINDA TUNAUSHINDANIA USHINDI WAKE
1.Kutii na Kupinga : Yakobo 4:7-8, 1Petro 5:7-9
Wakati 
wote kaa chini ya mamlaka ya Yesu. Tenda asemayo, ishi kwa upendo, Kwa 
kufanya hivi mamlaka yake itadhihirika kwako ukimpinga Shetani, 
atakimbia. Ukipinga upingamizi wake atakimbia.
2.Kufahamu uwanja wa Mapambano: 2Wakorintho 11:3, 2Wakorintho 10:3-4
Kanuni
 moja ya vita ni kujua adui anapigania wapi. Shetani hupingana nasi kwa 
kupitia mawazo na fikra zetu. Hulenga mfumo wa mawazo. Ukiweza kumshinda
 katika mawazo yako hataweza kukupata. Akikupata mawazo yako amekupata 
maisha yako. Mpinge katika mawazo kwa kusema kitu kwa kinywa, si kwa 
kuwaza neno tu, bali kwa kulisema. Usemapo neno kinywani linashinda mawazoni.
3.Kufahamu Silaha Yako: Waefeso 6:17
Maandiko
 yameonyesha silaha kadhaa, silaha zote zinamsingi wa Neno la Mungu. 
Kama vile meli inavyotegemea nanga, wakati wa mawimbi, Neno lisiache 
kutoka kinywani mwako, wakati wa misukosuko tu, linashinda tu. Luka 4:1 
-11, inaonyesha Yesu alidumu kusema Neno la Mungu, Shetani alipokuwa 
akimjaribu au kumpinga. Alidumu na Neno kinywani mpaka Ibilisi 
akamwacha, kisha malaika wakamuudumia. Udumupo kusema neno mpinzani atakuacha mbinguni watakuudumia.
4.  Walio Upande Wako: Warumi 8:31, Zaburi 118:7
Katika 
mawazo yako mwone Mungu yuko upande wako, Shetani anayekuchukia 
ameshindwa (Zaburi 118:7).  Malaika walio upande wako ni wengi kuliko 
mashetani. Kanisa la Yesu au waliookoka wako upande wako, wana mamlaka 
kubwa kuliko Shetani.  Yesu aliye ndani yako ni mkuu kuliko Shetani!
5. Kufahamu Nafasi Yako: Waefeso 2:5-6
Yesu 
yupo juu ya kila kitu (Waefeso 1:19-23), Upo juu ya kila kitu pamoja 
naye (Waefeso 2:5-6). Mashetani wote na hila zao zipo chini ya kinywa 
chako, Yaani neno usemalo.
6. Kukaa katika Roho: Waefeso 6:18, Yohana 4:23
Unamshinda
 Shetani kwa kukaa katika Roho Mtakatifu. Unapokaa katika ufunuo wa Roho
 katika kulijua neno, Unapodumu kuomba kwa Roho Mtakatifu, Unapoishi kwa
 tunda la Roho na si matendo ya mwili.  Unapomwabudu Mungu kwa nguvu za 
Roho Mtakatifu. Wakati wote unapokuwa na ushirika na Roho kwa kuongea 
naye, ni wakati kwa kumshinda adui.
7. Kukaa katika Agano: Yohana 10:28, Yohana 6:37
Shetani
 hawezi kukutoa katika agano lako na Mungu kwa njia ya Yesu.  Upo 
mikononi mwa Yesu hakuna awezaye kukutoa hata kwa hila, mtazame Yesu 
aliye ndani yako na kushinda.
Kumshinda Shetani ni Kushinda Woga
“Kwa
 kuwa hamkupokea tena roho ya utumwa iletayo hofu; bali mlipokea roho ya
 kufanywa wana, ambayo kwa hiyo twalia Aba, yaani Baba”
(Warumi 8:15)
 Zamani,
 nyakati za biblia watumwa hawakuruhusiwa kuwaita bwana zao “Aba” yaani 
baba mpendwa. Watumwa waliokuwa chini ya mwanamke hawakuruhusiwa kumwita
 “Imma”. Watumwa na bwana zao walihusiana kwa misingi ya hofu.  Watoto 
hawakuwa na hofu waliwaita baba zao “Aba” na mama zao “Imma”, kwa 
watumwa haikuwa hivyo.
Nguvu ya  Shetani
Roho ya kitumwa ni roho ya dhambi, “…Kila atendaye dhambi ni mtumwa wa dhambi.” (Yohana 8:34). Roho hii  ni chanzo cha woga, au hofu.  Adamu alipotenda dhambi tu, alisema yafuyatayo mbele za Mungu, “…Nilisikia sauti yako bustanini, nikaogopa kwa kuwa mimi ni uchi…”
 (Mwanzo 3:10). Adamu alipotenda dhambi alikufa, alitengwa na Mungu, 
hakufa tu!  Bali pia alikuwa mtumwa kwasababu ya roho ya woga, 
iliyoambatana na dhambi.  Akaanza kumkimbia Mungu! Mwanzoni alimwona 
kama Aba, sasa akaanza kumwogopa kama mtumwa! Wanadamu wote tukageuka 
kuwa watumwa wa ibilisi kutokana na dhambi ya Adamu, Shetani akatutawala
 kwa woga wa mauti, tukawa watumwa.
Yesu Ameondoa Woga
Woga
 uliingia duniani kwa njia ya Adamu aliyekuwa katika mwili. Woga 
unaondoka katika maisha yako kwa Yesu aliyekuja katika mwili.  Yesu 
amemharibu Shetani aliyetutawala kwa woga wa mauti, Akatuacha huru 
(Waebrania 2:14). Katika Yesu Mungu amekuwa Baba yetu, tunamwita Aba kwa
 kuwa si watumwa tena wa Shetani na dhambi kwa njia ya Yesu.
WOGA
 NI MLANGO WA SHETANI KUMWINGIA MTU NA KUMTAWALA.  IKIWA UMEMPA YESU 
MAISHA YAKO, YESU AMEUFUNGA MLANGO HUO. UKIMTAZAMA YEYE NA KUMTAMKA YEYE
 KATIKA MAZINGIRA YA WOGA YANAYOKUZUNGUKA  SHETANI HATAPATA NAFASI.
Vyanzo vya Woga
1.     Kuogopa Mambo Yajayo: Kwa
 mfano utaishije na uchumi unazidi kuwa mbaya. Unaweza kupata mawazo 
yanayoongea na kukuuliza utaishije, bila shaka itakuwa ni Shetani 
anapandikiza woga ndani yako, ili  kutafuta mlango katika maisha 
yako. Dawa ya woga huu ni kujua Yesu ni wa kwanza na wa mwisho, yupo 
sasa, amekuokoa na ameshashika na maisha yako yajayo! (Ufunuo 1:18).
2.      Kuogopa Kifo: Maandiko
 yanasema uhai wetu umefichwa katika Kristo. Shetani hawezi kuupata uhai
 wako, labda akaunyang’anye kwa Yesu. Hauishi kwa nafsi yako unaishi kwa
 njia ya Yesu, sema na kuwaza hivyo, woga wa kifo utakimbia. Woga huu ni
 woga wa hatari, wenyewe ni kifo! Ukiona unaogopa kifo shindana haraka 
kama unashindana na Shetani. Kwa kutamka uhai wako ndani ya Yesu 
(Wakolosai 2:1-3).
3.      Kuogopa Kushindwa:
 Kuogopa kushindwa ni kama vile, kuogopa kuomba kazi kwa kuwa hutaiweza,
 kuogopa mtihani kwa kuwa hutafaulu nk.  Kuogopa kushindwa ni kujiandaa 
kushindwa.
4.      Kuogopa Watu: Woga mwingine mbaya ni kuogopa watu. Kila utakacho kufanya unafikiria watu kwanza, woga wa namna hii ni mtego, “Kuwaogopa wanadamu huleta mtego bali amtumainiye Bwana atakuwa salama.” (Mithali 29:25). Woga huu ujapo tamka tumaini lako kwa Mungu zaidi ya watu, utatoka katika mtego wa Shetani.
5.      Kuogopa Yasiyojulikana: Mara
 nyingine unaweza kujikuta unaogopa kitu kisichojulikana; Au unaogopa 
kila kitu; Unaogopa watu, ukipanda basi unaogopa kiti cha basi kukalia; 
unaogopa matairi ya basi yatapasuka! itabidi uongee na woga huo kama 
roho.  Kama kiumbe cha kishetani; kama pepo. Uiamuru itoke kwa jina la 
Yesu, katika nafsi yako, pia uambie roho hiyo, hujapewa roho ya woga 
(2Timoteo 1:7).
Badilisha
 mfumo wako wa kufikiri, utabadilisha mfumo wako wa mitazamo, baada ya 
hapo utajijengea ngome ya kutoogopa na kuangusha ngome ya woga. Ngome ya
 woga ni ngome ya kushindwa, kutoogopa kwa njia ya Yesu ni kushinda.
Wakati wote jenga ngome ya kutoogopa kwa kusema maneno haya:
Isaya 51:12
Zaburi 118:6
Waebrania 13:5-6
Mathayo 10:28
Mithali 1:33
2Timoteo 1:7
Ufunuo 1:18
UPINGAPO WOGA UNAMPINGA SHETANI
Mungu  na akubariki wewe na familia yako na damu ya Yesu ikutetee na kukushindia  kwa hali zote unazo pitia.
wako mtumishi Mecky leo.
Comments
Post a Comment